Akijibu swali kwa niaba ya waziri wa Katiba na Sheria, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samwel Sitta alisema masuala ya mirathi nchini hutawaliwa na sheria tatu. Alizitaja sheria hizo kuwa ni za kimila ambazo hutumika ikiwa marehemu aliishi kwa kufuata mila na desturi za kabila lake, sheria ya kiislamu ambayo hutumika ikiwa marehemu alikuwa mfuasi wa dini hiyo na sheria ya Urithi ya India ya mwa 1865 iliyopokelewa na mahakama za Tanganyika na ambayo hutumika ikiwa marehemu hakuwa muumini wa dini ya kiislamu au hakuwa akifuata mila na desturi za kabila lake. Alisema serikali haina mamlaka ya kubatilisha sheria za kidini hata kama zitaonekana kuwa zina mwelekeo wa ukandamizaji. Kwa upande wa sheria za kimila Mheshimiwa Sitta alisema mahakama zina uwezo wa kuzitangaza sheria hizo kuwa ni batili endapo zitakuwa zinakiuka misingi ya haki iliyomo katika Katiba au sheria za nchi. Alisema katiba ya nchi ni sheria mama na haiko chini ya mila kwa kuwa ndani ya katiba misingi ya kuheshimu dini imewekwa. Aliongeza kuwa katiba imetoa uhuru wa kila mmoja kuwa na dini yake. Mheshimiwa Sitta amewatahadharisha walio katika ndoa wakiwa na dini tofauti kuwa masharti ya mirathi katika dini ya kiislamu ndiyo yatakayotumika wakati wa kudai mirathi. Mheshimiwa Sitta alisema suala la mirathi litaendelea kuwa na utata kwa kuwa bado tunatawaliwa na mfumo dume ambao si mzuri hivyo wananchi wanapaswa kuendelea kuelimishwa ili kuondokana na mfume dume. |
Comments
Post a Comment