KWAKO MHESHIMIWA RAIS KUTOKA KWA MWANANCHI WAKO MATUKIO CHUMA.

Kwa heshima na wingi wake wa taadhima, niruhusu nikusalimu, kutoka nchi iliyojaaliwa na ikawa jadidu, rasilimali tika zingekuwa matunda labda zingali tamu zikazidi zabibu, palipo mrefu Mlima barani Afrika, ukastaajabisha Dunia, uitwao Kilimanjaro, hivi karibuni Ngorongoro nayo Serengeti asilia maajabu kujuayo, nikipungwa na upepo maridhawa marashi ya yake Pemba na Unguja ikaitwa visiwa Zanzibar, mapango Amboni, nikijivinjari wingi wa sokwe Gombeni, Udzungwa, Saadani, Mahale nako Selous hata walipobwaga yao mioyo pakaitwa Bagamoyo, Tanzania iliyojaa wingi wa heri, maliasili, malighafi na ukarimu usiokinai, NAKUSALIMU,

Kwako Mheshimiwa Rais, Alipouwawa mwananchi kule katika kata ya Ubaruku Wilaya ya Mbarali Mkoani Mbeya kwa kutetea maslahi aitwae Mwekezaji, apewae lukuki haki, akapewa mauti mzawa akidai iliyo dhihiri yenye shubiri haki, Mtoto Juma Malomo miaka kumi na miwili tu, labda alie na wingi wa ndoto kutimiza tena kwa maslahi ya lake Taifa akwamishwapo, risasi kwa kiumbe hiki kule Keko Molemo wilaya Temeke,  tarehe 24 Oktoba 2010 ikawa mwanzo wa kutunukiwa ulemavu usio rasmi, mzigo ulio mzigo wala si mithili bali zaidi ya zigo la kuni, masikini aulizwapo ndoto zake bado zingali zilizo huku machozi ya uchungu yammiminikapo kuwa Rais ama Rubani irukapo ndege angani apatapo angalizo,

Polepole yakaanza kule visiwani palipo wingi wa mwani ila tukafunga macho tukajifanya tumelevywa na wingi wa nzuri nukia yake marashi yakaitwa karafuu, tukasahau ya 1995, ikaja 2000, 2005 mengine mengi historiani, tukasingizia udini, mara ugaidi hata kuwaita watufanyao watwana tukiendelea kuwavika ubwana, yakaanzwa makanisa, wakafuatia viongozi wa dini ukristuni, ikawa tindikali, mara mapanga, bisibisi, mauaji yasiyo mithili, ikahamia islamuni nao kadhia ikawahimi utekaji, misukosuko na hata madhara kuyahini, wakatangazwa watuhumiwa waliokamatwa na kuangazwa kwa mbwembwe zisizo kifani, mwishowe ikawa SINTOFAHAMU, mashtaka yaliyokosa weledi bali wingi labda wa dhihaka ya haki kama si kebehi, walioitwa wajinai ikafika onekana mashtaka wala yaliyotangazwa kwa hakiki yakakosa STAHILI?

Funika kombe mwanaharamu apite, yakaanza nukia Arusha, hatujastahi ikawa vurugu zizizokifa Iringa, Mbeya, Mtwara huko gesi nako ifika (penginepo waweza nikumbusha Mheshimiwa Rais maana labda nyingine ripoti kwetu sie pangu pakavu hazijotufika)? Je tunahitaji mgeni aje kwa kumchezea sindimba, kumpigia gwaride na hotuba nzuri kumsomea kutuambia kuwa tuelekeako siko na 2015 yaweza kuwa maafa kwa sababu tunaachia sio tu nyufa bali pandikizi za chuki, ubinafsi, uzandiki, ubadhirifu, uhasama, unafiki na wingi wa dhuluma pasipo haki wala huruma? Je twahitaji huyo ili tuje nae tumuandike kwenye vitabu vilivyotukuka tele vya historia kwamba alikuja fulani kutoka nchi ile kubwa tamalani, alieona mbali na akawa wa kwanza kuona yatakayojiri katika nchi yetu isiyo ongofu bali tuliyoionea fahari kwa miaka nenda iliyo zaidi ya kenda kama kisiwa cha Amani?

Kwako Mheshimiwa Rais,
Kulipo makao makuu ya kuanzia Afrika yake Mashariki, Afrika na hata ofisi kuu kadha wa kadha ukaitwa Umoja wa yake Mataifa, ni taifa lipi ama mji upi usiotolea macho paitwapo Arusha, leo hii kimya kikatawala vinywa pasipo kunusuru hadhi ya mahala hapo HUSIKA? hivi tunaziona gharama zake iwapo shughuli za yote haya makao husika, utalii nao ukafikwa? UWAPI MHESHIMIWA RAIS?
Ilianza kipindi kileeee, ikasemwa ni kikundi kileeee, haya tukasimikwa imani ni siasani, upepo tu wala usio nishani, stahilahi zetu nafsi buuu ikahamia nako ibadani? yalianza maandamano sasa imekuwa kwenye ulipo labda kila mkusanyikoni basi hata palipo mazikoni?

Kwako Mheshimiwa Rais,
Kwa uchaguzi uliokuweka madarakani, ni uaminifu wa jamii iliyo imani na kukupa wewe unahodha kwa kuamini tuendako tutafika, Iweje leo, chombo kiendapo mrama, upepo uzidipo kadhia na wala si tu kwa kuona mbali udhia, wangaliao wasaidizi wa chombo wakaweka uadilifu kando, maslahi ya Taifa yakawekwa kwa kibindo na fedhuri, kebehi na dhihaka isiyo na chembe ya kweli kutaka kutamka kuwa hakuna kilicho mrama wala chombo hakiendi zama,
Naam, akaitwa Mkuu kati ya wengine wengi Mawaziri, heri akaendelea kukaa kimya akapewa sifa ikaitwa asiye na makuu, mnyenyekevu kuliko kujaribu kufungua chake kimya akayatoa maneno yanayokifu yakakosa UCHANGANUZI YAKINIFU, eti mtoto wa mkulima, yupi nchi hii hiyo stamili asiyoihifu hata kama si yeye basi katika asili aliyoidhifu? Na hajaanza leo kila akurupukako na yale hadharani kuyawapo, alianza kwa ndugu zetu wenye ulemavu wa zao ngozi, akarudi mbio KUANGUA KILIO? haya sasa kipi kifuatacho? ALIFANYA ama KUTEKELEZA yapi baada ya hapo? wakiwindwa mithili ya kujificha digidigi, kukatwa vyao viungo kama si mauti kuwadhihaki? MHESHIMIWA RAIS TUNAHITAJI WAZIRI MKUU NA WATENDAJI KWA VITENDO VILIVYOSIMAMIA HAKI, TUMECHOSHWA NA MANENO YASIYO TIJA BALI TAMALAKI, LABDA KILIMO KINAMSTAHILI ZAIDI, CHONDECHONDE TUNATAKA MTENDAJI,

Kwako Mheshimiwa Rais,
Uwapi wetu utaifa, nani aliyesema kila mmoja haki yake itapimwa kwa itikadi, utiifu na upofu wa hali halisi bali uanachama wa chama au kada fulani, je kweli hatutambui mamilioni ya walio wananchi wasio na chama na wengi waliochoshwa na ahadi na mbwembwe za itikadi zilizokosa utekelezwaji, uendelezaji bali kila ifikapo kipindi kunadiwa kwa midundo, shamirisho zisizo komo wala uhakiki ushindi ufikiwapo?

Namuwaza mwananchi kule Mbinga, Muheza matunda aliyowekeza kuvuna shambani muda ukifika kumuozea nyumbani na kwa machache bei ya chini kuuza shurutika, kule Wete ahangaikae na jahazi mkono mmoja kupiga kadhia mwingine samaki chomboni kumvizia, vijijini mpaka mashambani, maziwani mpaka baharini, ukadhani mjini afadhali waishio maisha yasiyo tija wala staha wengi na hali za kustaajabisha,

Nataka kucheza bado kwa furaha kuondoa wangu wingi wa mawazo na tafakuri, msongo wa mawazo HATIMA YA LANGU TAIFA KUNIJAA ,mdundo ulipo mdundiko (NISIJE TAHARUKI KUGUNDUA KUMBE NI MLIPUKO LIKAITWA BOMU), wapi nijitupe na kujimwaya iitwayo sindimba, nicheze kwa fahari ritungu, huku taratibu nikinesa nisikiapo vanga, mnanda, mganda kwa mbali nasikia kibati nipisheni niingie katikati, kwetu Tanzania kwa nini mnataka kuninyima asili na wingi wa amani, fahari, utulivu, tukapanga endelevu maendeleo KUJIVUNIA?

Japo labda chozi latiririka, nikitafakari tulikotoka, tulikopita na sasa tuelekapo kama meli iliyokumbwa na wingi wa upepo na kukosa stamilivu himili, lakini naamini bado hatujachelewa ingali tu wewe nahodha uliekabidhiwa chombo utapoamua si kusikiliza nyimbo nzuri za sifa na wingi wa tukufu ripoti za utekelezaji usio na chachu endelevu bali kutafakari zile pia zilizo chungu, pinganifu na zilizojaa mapendekezo yakinifu, UWAPI MHESHIMIWA RAIS?

Ndimi Mwananchi Wako,

Comments